Saturday, September 14, 2013

TASAF YAMWAGA BILION 1.7 KATIKA MIRADI MBALIMBALI WILAYA YA NANYUMBU MKOA WA MTWARA.






 Vijana Kikundi cha sanaa cha mjini mwema wakionesha umahiri wao mbele ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais mahusiano na Uratibu Stevin Wasira aliyefika katika kijiji hicho kwa ajili ya kukagua mradi wa miti kwa ajili ya kulinda vyanzo vya maji
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais mahusiano na Uratibu Stevin Wasira akisalimiana na viongozi wa kijiji cha Michiga ndani ya wilaya ya Nanyumbu.
 Wananchi wa Msinyasi wakimsikiliza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais mahusiano na Uratibu Stevin Wasira(hayupo pichani) baada ya kukagua mradi wa barabara iliyounganisha kati ya kijiji cha magomeni na msinyasi yenye urefu wa KM 9.8
 Moja ya ufadhili wa TASAF wa umeme wa jua katika shule ya sekondari ya Sengenya
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu Stevin Wasira akisikiliza risala ya kikundi cha wajane na wagane wa kikundi cha ufugaji kuku katika kijiji cha ngalinje.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais mahusiano na Uratibu Stevin Wasiraakimsikiliza mjane Hadija Mrope kabla ya kukagua mradi wa ufugaji wa kuku uliofadhiliwa na TASAF katika kijiji cha Ngalinje Wilaya ya Nanyumbu Mkoa wa Mtwara.
 Watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya nanyumbu wakimsilikiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais mahusiano na Uratibu Stevin Wasira kwenye ukumbi wa mikutano wa mkuu wa wilaya.
 Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu Mkoa wa Mtwara Festo Kiswaga akimkaribisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais mahusiano na Uratibu Stevin Wasira alipowasili wilayani humo kwa ajili ya ziara ya siku moja kukagua na kujionea shughuli za maendeleo ya wananchi kwa ufadhili wa TASAF.



Na Thomas Dominick,
Nanyumbu

Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF)  awamu ya pili umetoa jumla ya Tshs Bilioni  1.7 kwa ajili ya kufadhili miradi 85 katika vijiji mbalimbali vya Wilaya ya Nanyumbu, Mkoa wa Mtwara.

Akitoa taarifa fupi ya maendeleo ya wilaya hiyo kwa Waziri wa Nchi  ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu Stevin Wasira aliyekuwa katika ziara ya kukagua miradi iliyofadhiliwa na TASAF Mkuu wa wilaya Festo Kiswaga alisema kuwa TASAF imesaidia kuinua maisha ya wananchi ya wilaya hiyo katika nyanja mbalimbali.

Kiswaga alisema kuwa jumla ya miradi 75 imekamilika na miradi ambayo ipo katika hatua ya utekelezaji ni miradi 10 iliyoanza Julai mwaka huu na pia kuna miradi 14 inayosubiri fedha kutoka TASAF.

“Miradi iliyokuwa katika hatua ya utekelezaji ni miradi sita ya ujenzi wa barabara, miradi mitatu ya uhifadhi wa mazingira na mradi mmoja wa hifadhi msitu shirikishi,”alisema Kiswaga.

Pia alisema kuwa wilaya hiyo inakabiliwa na upungufu mkubwa wa vyumba vya madarasa, nyumbza za walimu, zahanati na mabweni kwa shule za sekondari.

“Hivyo watoto wanasoma katika mazingira magumu na pia walimu kufundisha katika mazingira magumu na duni hii inachangia kushuka kwa elimu,” alisema.

Mkuu huyo wa wilaya alitumia fursa hiyo kuiomba TASAF ione uwezekano wa kuiwezesha Halmashauri hiyo kutatua tatizo hilo kwani serikali inajitahidi kuwashirikisha wananchi katika mipango mbalimbali ya maendeleo.

Naye Waziri Wasira aliwaomba wananchi kutumia fursa zinazotolewa na serikali ili kuweza kujiletea maendeleo yao wenyewe na kujikwamua kutoka katika umasikini uliokithiri katika jamii.

“Mipango ya TASAF ni endelevu ili kuwainua wananchi wetu kutoka katika umasikini na kuishi maisha  mazuri pia tunawashauri wataalamu wetu kuwa karibu na wananchi kuwapatia mafunzo bora ya kilimo, ufugaji na uzalishaji mali,”alisema Wasira  

Wasira aliwaomba viongozi wa TASAF alioambatana katika ziara hiyo wanatakiwa kujifunza na kuona matatizo yanayowakabili wananchi na kufikiria zaidi familia maskini.

Miradi aliyotembelea ni pamoja na kikundi cha ufugaji kuku cha wajane na wagane kilichopo kijiji cha Ngalinje, ujenzi wa barabara kuunganisha kijiji cha magomeni na msinyasi na barabara yenye urefu wa Km 4 inayounganisha kitongoji cha Mikangaula na kijiji cha Nakopi.

Miradi mingine ni ujenzi wa masijala ya kutoa hati miliki katika kijiji cha michiga na  mradi wa kupanda miti kwenye vyanzo vya maji katika kijiji cha Nangomba ambapo kwa sasa kuna vitalu takribani 20 na wanatarajia kupanda miti hiyo mwezi Desemba mwaka huu.


0 comments:

Post a Comment