Friday, December 7, 2012

POLISI MARA YAKANUSHA UVUMI WA WATU 15 MKOANI HUMO KUCHINJWA.


Baadhi ya waandishi wa habari wa Mkoa Mara wakiwa ndani ya ofisi ya Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa huo, Japhet Lusingu wakisubiria taarifa muhimu juu ya uvumi ulioenea nchi nzima wa mauaji wa wananchi wa mkoa huo. 


 Mwandishi Mkongwe Mkoani Mara Maxmilian Ngesi (mwenye shati la njano) akisoma meseji kwenye simu yake anayetazamana naye ni Shomari Binda na anayechukua picha za video ni Dick Mohamed mwakilishi wa Star TV Mkoani hapo wakati akiwa ndani ya ofisi ya Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa huo, Japhet Lusingu.

 
 Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa huo, Japhet Lusingu akitoa taarifa kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) juu ya taarifa za uzushi zilizozagaa nchi nzima kwa kusambazwa kwa wananchi wa mkoa huo pamoja na vyombo vya habari kuwa zaidi ya watu 15 wamechinjwa na vichwa vyao kuchukuliwa na watu wasiojulikana.

*watakaobainika kusambaza uongo huo kukiona
*waandishi wa habari wapashwa 

Na Thomas Dominick,
Mara

Jeshi la Polisi Mkoani Mara limekanusha uvumi wa kutishia wananchi toka baadhi  wananchi wenye nia mbaya na vyombo vya habari nchini kutangaza na kusambaza kuwa ndani ya mwezi mmoja watu 15 wameuwawa kwa kuchinjwa.

Akizungumza na waandishi wa habari katika mkutano maalumu ofisini kwake, Kaimu Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa huo, Japhet Lusingu alisema kuwa kumekua na uvumi kuwa katika Mkoa wa huo wananchi wamekuwa wakichinjwa na tayari watu 15 wameuwawa kwa kuchinjwa kitu ambacho ni uongo.

Kamanda Lusingu alisema kutokana na uvumi huo wamekua wakipokea simu toka kwa wananchi na viongozi ndani ya Manspaa ya Musoma katika kata ya nyakato kwamba kuna mwanafunzi ameonekana ameuwawa kwa kukatwa kichwa katika makaburi ya Musoma bus na jeshi la polisi likifuatilia wanakuta ni taarifa za uongo na za kuwatisha wananchi.

Alisema kuwa matukio mawili ndiyo yaliyoripotiwa ambapo wanawake wawili waliuawa  kati yao ni Blandina Peru (28) mkazi wa kijiji cha Mahare, kata ya Etaro ambapo aliuwawa Desemba 2 mwaka huu kwa kukatwa koromeo na kubakwa na wauaji kabla ya kumuua wakati akiwa porini akikata kuni na watuhumiwa wa tukio hilo bado hawajakamatwa.

Tukio la pili lilitokea Kabegi kata ya Nyakatende wilayani butiama ambapo Sabina Mkireri (44) mkazi wa kijiji cha kiemba aliwawa kwa kuchinjwa shingo na kichwa chake kuchukuliwa na watu wasiojulikana katika kijiji cha kabegi na watu sita wanashikiliwa na jeshi la polisi kwa mahojiano.

Kutokana na uvumi huo amewatoa hofu wananchi  juu ya mauaji hayo na kuwatahadharisha akina mama hasa maeneo ya vijijini wanapokua katika shughuli zao za kilimo na utafutaji wa kuni wawe waangalifu na watoe taarifa mapema wanaposhuku jambo lolote lisilo lakawaida.

“Nachukua nafasi hii kuwatoa hofu wananchi juu ya uvumi uliozagaa wa mauaji hayo na nawatahadharisha akina mama hasa maeneo ya vijijini wanapokua katika shughuli zao za kilimo na utafutaji wa kuni wawe waangalifu na watoe taarifa mapema wanaposhuku jambo lolote lisilo la kawaida,”alisema Lusingu.

Kwa upande mwingine Jeshi hilo limewaomba waandishi wa habari kupata taarifa kutoka kwenye vyanzo husika pia kwa watu ambao wanaoanzisha uvumi wakibainika wanatoa habari za uvumi hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Aliongeza kuwa kwa sasa wanaendelea na msako maeneo mbalimbali ya manispaa ya Musoma na wilaya ya butiama ambapo kuna watu watano wanashikiliwa na jeshi hilo kwa kwa makosa yakupatikana na pombe haramu ya gongo na wengine wanashikiliwa kwa kupatikana na bangi na wote watafikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.

Mwisho


 


0 comments:

Post a Comment